BONGO CELEBRITY

All You Wanted To Know But Didn’t Know How and Where

“TUUKATAE UFISADI”-DR.SLAA January, 27, 2008

Filed under: Serikali/Uongozi,Sheria,Siasa,Tanzania/Zanzibar — bongocelebrity @ 1:13 PM

Jina la Dr.Willibrod Peter Slaa (pichani),Katibu Mkuu wa CHADEMA na Mbunge wa Karatu, hivi sasa linaweza kuwa jina ambalo linatajwa zaidi kushinda lingine lolote katika anga za kisiasa nchini Tanzania.Wananchi wengi wanamuongelea kama kiongozi shujaa,aliye tayari kudiriki kufanya au kusema chochote katika kutetea maslahi ya wananchi hususani wale wanaoitwa “wa kawaida” na wenye hali duni za kimaisha.Angekuwa anaishi katika nchi za magharibi,Dr.Slaa angeitwa “whistleblower” nambari wani jina ambalo hupewa mtu anayeamua kuwa mkakamavu na kukemea mienendo mibaya na isiyofaa ya watu walioko kwenye madaraka fulani nk, potelea mbali kinachoweza kumtokea kutokana na ujasiri huo.

Kwanini jina la Dr.Wilbrod Slaa liwe vinywani mwa watanzania wengi hivi sasa?Jibu ni rahisi;ni kutokana na mchango wake katika kufichua “ufisadi” uliokuwa unafanyika katika Benki Kuu ya Tanzania(BOT) na mambo mengi mengineyo ambayo anahisi yanakwenda visivyo.

Ingawa umaarufu wa Dr.Slaa haujaanzia na suala la BOT,ni wazi kwamba sakata hili ndilo limefanya jina lake liwe miongoni mwa majina maarufu sio tu kutoka kambi ya upinzani bali katika anga za wanasiasa kote nchini Tanzania.

Lakini Dr.Slaa ni nani?Anatokea wapi?Wangapi wanafahamu alikuwa akifanya nini kabla hajaingia kwenye siasa? Tangu ameingia kwenye siasa amepata mafanikio gani? Anasemaje kuhusu sakata zima la BOT?Ameridhika na maamuzi yaliyochukuliwa na Rais Kikwete?Ana ujumbe gani kwa wananchi?Ili kupata majibu ya maswali hayo na mengineyo, hivi karibuni tulipata fursa ya kufanya naye mahojiano rasmi.Fuatana nasi katika mahojiano yafuatayo;

BC: Dr.Slaa karibu sana ndani ya www.bongocelebrity.com. Ni heshima kwetu kupata nafasi hii ya kufanya nawe mahojiano.Jambo la kwanza kabisa ambalo tunaamini wasomaji wetu wangependa kujua ni kuhusu historia yako. Je, unaweza kutueleza ulizaliwa wapi,lini,ukasomea wapi mpaka kufikia hadhi ya udaktari wa falsafa?

 

WS:Historia fupi, nilizaliwa Kwermusl, Mbulu, Tanzania, tarehe 29.10.1948.Lakini ili kukidhi haja ya swali hili zima,labda tuambatanishe CV au BIODATA yangu kama ifuatavyo;

CURICULUM VITAE(BIODATA)

Full Name: Willibord Peter Slaa.

Date and Place of Birth: 29.10.1948,Kwermusl,Mbulu,Tanzania.

EDUCATION:

PRIMARY: 1958-1961 Kwermusl

1962-1965 Karatu Middle School.

SECONDARY: 1966-1969 Dunguyi Seminary

1970-1971 Itaga Seminary

PHILOSOPHY:

1972-1973 Kibosho Seminary

THEOLOGY:

1974-1977 Kipalapala Seminary

1974-1976 Makerere University,Diploma,Theology

HIGHER EDUCATION:

1979-1981 Pontifical Urba University,Rome,JCD(summa cum laude)

1980-1980 ADV.Diploma-Socio-Political Studies,Koln,Germany(KAF)

1981-1981 St.Thomas Aquinas University,Rome,AD.Diploma Rural Development

1985-1985 London COR.College, Principles and Practice of Management Certificate.

WORK EXPERIENCE:

2000-Todate Member of Parliament(MP),Karatu

1995-2000 Member of Parliament(MP),Karatu.

1991-1995 Executive Director,Tanzania Society for The Blind.

1986-1991 Secretary General,Tanzania Episcopal Conference(TEC)

1982-1986 Development Director,Diocese of Mbulu

1982-1986 Vicar General,Diocese of Mbulu

1977-1979 Development Director,Diocese of Mbulu (Catholic Priest 1977-1991)

MEMBERSHIP IN LOCAL AND INTERNATIONAL BODIES

2006-Todate: Deputy Leader,Official Opposition, Parliament of Tanzania

2000- Todate: Vice President, Forum of African Parliamentarians on Education( FAPED)

2004-Todate: Secretary General,CHADEMA.

2001-Todate: Member,Special Education Committee,MOEC/SADC.

2000-Todate: Shadow Minister,Legal and Constitutional Affairs.

1998-2004 Vice Chairman,CHADEMA

1998-2003 Chairman, Inter-Parliamentary Forum (SADC-PF)

1996-2000 Member,ACP-EU Joint Parliamentary Assembly

1994-Todate: Chairman,Comprehensive Community Based Rehabilitation Tanzania (CCBRT)

1992-1995 Secretart,National Prevention of Blindness Programs,MOH

1992-1995 Director,SLS General Trading Co.Ltd

INTERNATIONAL CONFERENCES

Attended numerous national and international conferences and workshops,presented papers and facilitated in a number of them including,IPU,SADC-PF and CPA organized workshops and conferences.

Attended numerous short courses and seminars both within and outside the country.

BC: Wanasiasa wengi wanasema kwamba waliingia kwenye siasa baada ya kukerwa na mambo fulani fulani wanayokuwa wanahisi hayaendi sawa kijamii,kisiasa au kiuchumi.Kama maelezo hayo yanafanana na historia yako kwenye siasa,ni jambo au mambo gani yalikufanya uingie kwenye siasa?Na tangu umeingia umeweza kuleta mabadiliko gani mpaka hivi sasa?

WS: Niliingia kisisasa mwaka 1995, bila kuwa na nia kabisa ya kuingia kwenye uongozi hasa ubunge japo kwa nafasi mbalimbali nimeshiriki shughuli za Kisiasa huko nyuma. Nimekuwa Katibu wa TANU Youth League nikiwa Kipalapala Seminary, na kufungua matawi mengi ya TANU wakati huo. Nimekuwa Katibu wa Shina la CCM, Tawi la Mambo ya Nje, Rome wakati nasoma Rome, 1980-81.

Niliingia kugombea ubunge baada ya Wazee wa Karatu kunifuata Dar-Es-Salaam, wa vyama vyote vilivyokuwepo wakati ule-CCM, Chadema, NCCR-Mageuzi. Nikaombwa nichague chama ninachokipenda, na kama ilivyokuwa kwa kila mmoja wakati ule nikaingia kupitia CCM. Nikashinda kwenye Kura za Maoni ndani ya CCM, lakini jina liliondolewa kimizengwe, kwa msingi kuwa “mimi si mwenzao”. Leo ninaelewa kilichomaanishwa, ni kweli kwa hali hii ya ufisadi mimi sikuwa mwenzao”. Sijutii kabisa, kuwa baada ya hapo niliingia Ubunge kupitia Chadema, nafasi pekee iliyokuwa wazi wakati huo. Sikuijua Chadema, sikuwa namfahamu Mzee Mtei, wala Katiba ya Chadema. Nadhani ni Mungu aliongoza hivyo kwa sababu anazofahamu mwenyewe, kwa wale wanaomwamini Mungu.

Jambo kubwa pekee lililokuwa linawakera Wananchi wa Karatu na kuja kuniomba ni : Maji. Karatu ni wilaya isiyo na mto hata mmoja wala maziwa yanayoweza kutumika na binadamu, japo tuna Lake Manyara upande wa Mashariki -Kusini na Lake Eyasi upande wa Magharibi. Wamekuwa wakiomba wapate miradi ya maji kwa miaka 30 lakini licha ya kuchangishwa mara kadhaa miradi hiyo ilishindikana kabisa. Kulikuwa pia na suala la Elimu hasa ya Sekondari na pia matatizo ya Huduma za Afya. Haya ndiyo mambo ya msingi kabisa waliyoomba kwangu wananchi wa Karatu wakitaka niwatangulie na kuwa wako tayari kufanya kazi nami katika hali na mali.

a) Nilipoingia tu, japo sikuwa na diwani, na mwenyekiti mmoja tu wa Kijiji kwa Tiket ya Chadema, na sikuwa na kitongoji hata kimoja, nilifanikiwa kupata msaada mkubwa wa maji kwa ajili ya mji wa Karatu na vijiji vitano vinavyoizunguka vya Ayalabe, Gongali, Gyekurum Arusha, Gyekurum Lambo, na Tloma kupitia shirika la MISEREOR la ujerumani kupitia Diocese of Mbulu, (Katoliki) ambao kwa muda mrefu nimekuwa nikifanya nao kazi na kujenga kuaminiana sana.

Hiki kilikuwa kipindi kigumu sana, kwani mradi huo uliwekewa mizengwe ya kila aina, mbinu za kutaka kuukwamishwa kutumia Katibu Tarafa, Mtendaji wa Kata, watendaji wa Halmashauri.

Hata hivyo, baada ya mapambano makali, kwa kushirikiana na Wananchi na bila Serikali ( ya Wilaya) nilifanikiwa kukamilisha mradi huo mwaka 2000. Siku maji yalipotoka wananchi waliomba dua, walisherehekea, na kuamini kumbe inawezekana. Kuanzia siku hiyo nimeendelea na kutafuta mbinu mbalimbali kupata miradi ya maji kwa ajili ya Wilaya nzima, na hadi leo, vijiji 35 vimepata maji ya uhakika ya Bomba hadi ngazi ya Kitongoji. Kazi iliyobaki ni ya usambazaji hadi karibu na wananchi, kupeleka DP kwa ukaribu wa mita 400 au chini ya hapo kufuatana na sera ya maji ya nchi, na kuingiza maji ndani (Domestic). Pia tumefanya jitihada ya kujenga mabwawa kadhaa kwa ajili ya matumizi ya binadamu na mifugo.

b) Kutokana na maendeleo hayo ambayo yalionekana dhahiri, Wananchi wa Karatu waliichagua Chadema mwaka 2000 na kuifanya CCM kuwa chama cha Upinzani. Yaani Mwenyekiti wa Halmashauri na wenyeviti wa Kamati zote wanatoka Chadema, kutokana na uwingi wa Chadema. Pia katika uchaguzi uliofuata wa Serikali za mitaa 2004, Chadema sasa ina vijiji vingi na vitongoji vingi vinavyoongozwa na Chadema. Wazo hili la CCM kuwa chama cha Upinzani limekuwa gumu sana kueleweka na CCM na serikali yake, hivyo wameendelea kuhujumu Serikali ya mitaa inayoongozwa na Chadema, lakini kwa kuwa tumekuwa imara na tumeendelea kuwa karibuni na wananchi, majaribio hayo yote yameanguka kwenye mwamba wa jiwe.

c) Kwa upande wa Elimu, mwaka 2000 Wilaya ya Karatu ilikuwa na shule moja tu ya wananchi, yaani AWET Sekondari. Lakini kwa Ilani na sera nzuri ya Chadema, tunapoongea leo, Wilaya ya Karatu inayo shule za Sekondari 25, na 3 ziko kwenye hatua ya mbalimbali ya ujenzi. Wakati Sera ya CCM ni shule za Sekondari katika ngazi ya Kata, Sera na Ilani ya Chadema Karatu ni kuwa na Sekondari katika ngazi ya kijiji, kwa vile Kata nyingi bado ni kubwa na shule za kata ni za kutwa hivyo zinakuwa mateso kwa watoto wetu. Zaidi ya nusu ya vijiji tayari vina shule za vijiji za Sekondari. Chadema kwa hili imetoa changamoto kwa Serikali ya CCM. Isitoshe, mwaka huu, 2008 watoto wote wanaotakiwa kuingia Sekondari waliotimiza vigezo, wameingia Sekondari, na bado tuna nafasi tupu 800 yaani tuna madara 20 zaidi kuliko watoto. Kitaifa watoto waliofaulu ni asilimia 51 wakati Karatu waliofaulu ni 54. Tatizo la msingi ni kuwa Serikali kuu inasua sua katika kutekeleza majukumu yake, mathalan upatikanaji wa waalimu ni tatizo kubwa, vifaa vya elimu na hata vitabu.

d) Huduma za Afya nayo ni eneo moja ambapo Chadema tumeonyesha njia. Sera na Ilani ya Chadema ilikuwa kujenga zahanati kila kijiji. Hadi leo ni vijiji 5 tu bado havina zahanati, na vijiji vyote au vimekamilisha ujenzi au viko kwenye hatua ya kumalizia ujenzi. Kutokana na changamoto hiyo, Serikali ya CCM pia sasa imetangaza bila kuwa na sera hiyo ujenzi wa Zahanati katika ngazi ya Kijiji kwa nchi nzima. Tatizo hapa ni Madaktari na manesi ambao ni jukumu la Serikali Kuu na upatikanaji wa uhakika wa madawa.

e) Jambo ambalo mara nyingi linafanyiwa porojo ni kuondoa manyanyaso ambayo wananchi walikuwa wanayapata wakati wa mfumo wa chama kimoja. Chadema Karatu tulipiga vita unyanyasaji wa aina yeyote. Mathalan, michango mingi isiyo ya kisheria inakusanywa kwa mabavu na kuwaumiza wananchi wa chini. Chadema tulipiga marufuku hayo. Ndipo Serikali ya CCM bila kujiandaa ikafuta kabisa kilichoitwa kodi ya Maendeleo. Kwa bahati mbaya walikurupuka bila kuandaa na wala kufanya “alternatives”, na sasa Serikali za mitaa ziko kwenye hali ngumu kujiendesha, na pia kuanzisha dhana mpya ya watu kutolipa kodi ya aina yeyote kabisa.Chadema tulipopiga marufuku kodi za manyanyaso tulitafuta vianzio visivyo na athari kwa mwananchi wa kawaida, wala visivyo na athari kwa uchumi mpana.

f) Miundo mbinu na kilimo ni eneo muhimu ambalo tumeweka mkazo kwa lengo la kupiga vita umaskini kabisa miongoni mwa watu wetu. Mikakati yetu ya kilimo, na jitihada za kutafuta vianzio vyetu vya fedha nje ya vile vya Serikali Kuu imeongeza sana fanaka katika mipango yetu mbalimbali.

BC: Tukiwa hapo hapo kwenye suala la historia yako.Wengi tunatambua kwamba siku za nyuma kabla hujaingia kwenye siasa ulikuwa padre au ulisomea upadre. Unaweza kutueleza kwanini uliacha upadri na kuwa mwanasiasa? Ulifukuzwa au uliacha kwa hiari? Una mke na watoto. Je, kanisa lilikuruhusu kuoa?

WS: Ni kweli nimekuwa Padre wa Kanisa Katoliki. Nimekuwa kiongozi wa ngazi ya juu sana ndani ya Kanisa kuanzia Jimboni kwangu ambapo nimekuwa Makamu wa Askofu, na Mkurugenzi wa Maendeleo, lakini pia nimekuwa Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu toka 1985 hadi 1991. Ni kweli hayo maswali yanaulizwa mara nyingi, kwa bahati mbaya si wengi wanaofahamu taratibu za kisheria ndani ya Kanisa Katoliki. Niliondoka mimi mwenyewe katika Upadre bila kushinikizwa na yeyote, wala kufukuzwa, wala hata kupewa onyo. Ni kweli kuna mambo ambayo mimi niliyakataa na kwa dhamira yangu nisingeliweza kuendelea, lakini nadhani hayo ni binafsi zaidi, na si mahali pake kuyaeleza. Nimetoka kwa kibali cha Kanisa, kwa utaratibu wa kisheria wa Kanisa Katoliki, ndiyo maana mimi sina tatizo wala ugomvi wa aina yeyote na Kanisa Katoliki na ninashiriki katika shughuli mbalimbali za Kanisa.

Nina Mke na watoto wawili, Emiliana Slaa na Linus Slaa, japo sijafunga ndoa kikanisa kwa utaratibu wa kawaida wa Kanisa Katoliki, pamoja na kuwa sina kipingamizi chochote kufanya hivyo kikanisa, ni uamuzi wangu na wa mke wangu na familia yetu.

BC: Baada ya mkutano wako wa hadhara pale MwembeYanga jijini Dar-es-salaam Septemba mwaka jana,vyombo vya habari karibuni vyote vilihofia kuandika ulichokisema na pia kuweka bayana orodha ya majina uliyoyataja.Unadhani kwanini vyombo vya habari viliogopa kufanya hivyo? Na wewe binafsi ulijisikia vipi kuona hali hiyo? Tukio lile lilimaanisha nini kwako kuhusiana na suala zima la uhuru wa vyombo vya habari nchini Tanzania?

WS: Nilijua kabisa kuwa vyombo vya Habari vinaogopa kuandika aina ya taarifa tuliyotoa na wenzangu pale Mwembe Yanga, hivyo sikushangaa. Nilifurahi sana nilipoona Gazeti dogo la Mwanahalisi, limethubutu, siyo tu kuandika majina na tuliyoeleza bali pia kuweka na picha yao. Tafsiri pekee ni kuwa vyombo vingi vilikosa ujasiri na uzalendo. Vilipenda kujilinda zaidi wasishitakiwe, wengine nao pia hawakuamini tuliyoyasema kama ni kweli na wala hawakwenda mbele zaidi kufanya utafiti wao kuthibitisha tulichosema. Hivyo, kuna mengi yanaweza kusemwa kuhusu vyombo vya habari na uhuru wa vyombo vya habari hapa Tanzania. Hali ni mbaya zaidi, unapokuta kuwa vyombo vingine vinamilikiwa na wanasiasa na hasa pale wamiliki wa vyombo hivyo wanapoguswa kwa namna moja au nyingine na tuhuma hizo.

Waandishi wa habari na vyombo vya habari ni muhimu sana katika ukombozi wa aina yeyote. Wanahitajiwa kuwa na ujasiri, kwani bila hivyo watakosa thubutu ya kwenda kwenye mstari wa mbele wa vita au mapambano kuripoti kinachojiri kama tulivyoona kwa waandishi wa CNN. Nampongeza sana Bwana Kubenea aliyejitosa, na kwa hakika ni shujaa wa kweli, na gazeti hilo dogo limeonyesha njia, naamini na mengine yatafuata njia.

BC: Baadhi ya wananchi,hususani kwenye kambi ya upinzani, wamekuwa wakihofia usalama wa maisha yako.Wengine wamekuwa wakitoa mapendekezo kwamba serikali haina budi kukupa ulinzi wa ziada. Je,wewe mwenyewe unahofia usalama wa maisha yako?Kama jibu ni hapana,kwanini?

WS: Ni kweli hisia hizo zipo na wengi wamenipa ushauri wa aina mbalimbali. Nawashukuru sana kwa kunipenda na kunijali. Hata hivyo, hatima ya yote, Usalama utatolewa tu na Mwenyezi Mungu. Tukumbuke kuwa John Kennedy ameuawa akiwa amezungukwa si tu na maaskari wa ulinzi bali pia na CIA na FBI. Wako waliokufa wamezungukwa na madaktari 30 au zaidi, lakini saa yao ilipofika waliondoka bila kuaga. Ninaacha Maisha yangu kwa Mwenyezi Mungu. Ninachukua tahadhari zote zinazoweza kuchukuliwa na binadamu, lakini kamwe sitaacha kufanya wajibu wangu, na kile ambacho dhamira yangu inataka nikifanye kwa kuhofia usalama na maisha yangu. Hatukuomba kuzaliwa na hatutaomba kuondoka humu duniani.

 

Kambi ya upinzani;kutoka kushoto kwenda kulia,Mwenyekiti wa TLP,Augustine Lyatonga Mrema,Mwenyekiti wa CUF,Prof.Ibrahim Lipumba,Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi,James Mbatia na Katibu Mkuu wa CHADEMA,Dr.Willibrod Peter Slaa.Anayeonekana nyumba kwa mbali katikati ya Mrema na Lipumba ni Maalim Seif Hamad,Katibu Mkuu CUF.

BC: Watu wengi wamejitokeza hadharani na kumpongeza Rais Kikwete kwa uamuzi wa kutengua ajira ya aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu,Daudi Balali.Pamoja na hayo,kumeibuka maswali kadha wa kadha kuhusu maneno kama “utenguzi wa ajira” nk. Tungependa kukuuliza maswali mawili juu ya hili.Kwanza,kwa mtazamo wako,Raisi amefanya kile ambacho ulikitegemea?Pili nini hasa maana ya maneno haya (utenguzi wa ajira) kwa jinsi ulivyoelewa wewe na pia kisheria?

WS: Ni wazi kabisa, msimamo wangu unajulikana na umenukuliwa na magezeti kadhaa:

1) Sijaona kabisa sababu ya kupongeza hatua ya Rais.Kwanza muda uliochukuliwa ni mrefu sana. Jambo hili limejenga matabaka katika nchi yetu. Kwa sheria iliyoko leo, ukituhumiwa unakamatwa, unapelekwa polisi, unawekwa lock up-au unapata mdhamana ambao ni haki yako isipokuwa kwa makosa fulani fulani tu. Lakini kwa tuhuma ya uwizi mkubwa masharti yanajulikana, mathalan kuchukuliwa kwa Passport yako ili usiweze kutoroka, kuweka mdhamana wa mali isiyohamishika kwa kiwango kilichowekwa na sheria nakadhalika, na uchunguzi unafuata baadaye. Hii ndiyo sheria ilivyo leo ( Sheria inayoenda Bungeni inabadilisha kidogo hali hiyo, uchunguzi unatangulia kabla ya kukamatwa). Haya yote hayakufanyika kwa mtuhumiwa wa Mabilioni, tena yaliyothibitishwa na wakaguzi, lakini ameaachwa ana tamalaki tu. Hi si ishara nzuri na wala si utawala bora kutengeneza matabaka kati ya wananchi wake Rais.

2) Hatua ya “kutengua” maana yake Dr.Balali bado ni mfanyikazi wa Serikali, ila tu uteuzi wake au nafasi yake kama Gavana imeondolewa. Wala Rais hajasema kama amesimamishwa kazi au vipi. Angalau basi Balali alitakiwa kusimamishwa kazi Serikalini na wakati Tuhuma zake zinapelekwa mahakamani. Lakini hilo halikufanyika, na kwa msingi huo inawezekana kabisa Balali anaendelea kupokea mshahara kamili, kwa vile hajasimamishwa utumishi wake Serikalini. Isipokuwa kama tutaelezwa vinginevyo, kwa taarifa tuliyonayo Balali ni mtumishi wa Serikali kabla ya kuwa Gavana, na utumishi huo haujasimamishwa.

3) Sijaridhika kabisa na hatua ya Rais, kwa vile, Tuhuma dhidi ya Balali nilizotoa Mwembe Yanga zinaenda zaidi ya Kasma “Vote” moja ya EPA ndani ya BOT.Ziko votes nyingi na ubadhirifu umetapakaa kwingi, kwa mfano fedha zilizolipwa Alex Stewart aliyekuwa anapata 1.9% ya Royalty yetu -ambayo ni 3%. Huu ni mkataba wa ajabu na kama kweli ilifanyika kihalali basi hii ni biashara kichaa kwa maelezo yeyote yale. Suala la malipo kwa Kampuni ya Mwananchi Gold Co halijaelezwa na wala Rais hajalieleza Taifa hatua gani za ziada zinaendelea kuchukuliwa, suala DEEP Green Finance Co halijaelezwa popote ambapo fedha za Umma toka Hazina/BOT zaidi ya 20 Billioni zimepelekwa kusikojulikana, ila kuna ushahidi wa kimazingira kuwa zilipelekwa kwenye uchaguzi mkuu wa 2005 kuisaidia CCM. Na mengine mengi tuliyoyasema Hizi zote ni fedha za Umma, na Rais hana mamlaka ya kuamua kutoa au kutotoa Taarifa kwa Umma. Ndiyo maana ninaendelea kushinikiza kuwa Tuhuma za Ubadhirifu bado mbichi na hatua zilizochukuliwa hazikidhi kabisa kwa kiwango chochote. Kwa bahati mbaya Watanzania wengi hawaelewi na hivyo wanaridhika tu na kidogo alichokifanya Rais. Tutampongeza Rais atakaposafisha uozo huu wote.

4) Rais alitakiwa kuwasimamisha vile vile wale wote waliohusika na uozo huu. Nimesema mara nyingi kuwa Balali si peke yake katika ubadhirifu na ufisadi huu. Wale wote wanatakiwa kuchukuliwa hatua.Tunaendelea kudai hawa wote wachukuliwe hatua akiwemo Gray Mgonja, ambaye pamoja na yote tuliyosema, anaendelea kuwa Mjumbe wa Bodi ya BOT kwa kofia yake ya kuwa Katibu Mkuu, Hazina. Ni muhimu Rais amwondoe, ili Katibu Mkuu mwingine aingie na kusaidiana na Gavana mpya kusaifisha nyumba. Vinginevyo tunatwanga maji kwenye kinu. Rais ameagiza Bodi ya BOT iwachukulie hatua wahusika wote, ni kweli hafahamu kuwa Gray Mgonja, aliyesaini nyaraka nyingi tu hahusiki kweli, hata kwa uzembe tu? Kama hajui basi tunatatizo kubwa zaidi kuliko tunavyofahamu na tunavyotaka kujiaminisha. Kwa hali hiyo basi ni dhahiri kuwa alilofanya Rais silo nililotegemea wala silo lililotegemewa na Watanzania wengi waelewa wa mambo.

BC: Hivi karibuni umekuwa ukilalamikia suala la serikali kutoiweka hadharani ripoti ya EPA kama ilivyowasilishwa serikalini na kampuni ya Ernst & Young.Unadhani kuna umuhimu gani kwa serikali kuiweka ripoti hiyo hadharani?

WS: Kuweka au kutoweka hadharani kwa Ripoti hiyo siyo hisani ya Rais wala ya Serikali. Jambo lolote lililofanyika kwa Kodi ya Wananchi linapaswa kufikishwa kwa wananchi hasa kama linahusu Tuhuma.

Kwanza serikali yenyewe ilitoa ahadi Bungeni kuwa itawekwa hadharani, kwa wananchi na kwa Wabunge. Itakuwa ajabu kama hata Wabunge hawatapewa. Itakuwa Serikali ya ajabu ambayo haiheshimu ahadi na kauli zake. Waziri Meghji naye pia aliahidi mara nyingi kuwa Taarifa ya Ernst and Young itatolewa hadharani leo kulikoni? Hii hatua ya sasa inazua utata mkubwa, kuna nini kinafichwa?

Pili taarifa hiyo ni muhimu kwa umma wa Watanzania kuona hasa nini kimeandikwa na nani anahusika. Nina sababu nzito ya kuamini kuwa viongozi wa Serikali waliosemwa katika Taarifa hiyo wameachwa nje, na ndiyo maana Serikali inapata kigugumizi katika kuweka Taarifa nzima hadharani. Hili haiisaidii Serikali bali inazidi kuichafua.

Ningependa kuamini Serikali imepata fundisho kwa jinsi ilivyoshughulikia suala hili, na sasa itakuwa makini zaidi, lakini inaelekea wenzetu hawa fundisho bado halijawaingia hata kidogo, na bado wana mawazo ya zamani kuwa Serikali inaweza kufanya inavyotaka. Serikali inayowajibika kwa Wananchi, inapaswa kuwa wazi (Transparent and Accountable). Tuko mbali sana na mambo hayo mawili ambayo ni msingi mkubwa sana wa Good Governance.

 

BC: Tofauti na hapo zamani,siku hizi taarifa zinasambaa kwa haraka sana.Shukrani kwa maendeleo ya kisayansi na kitekinolojia.Unadhani nini kitatokea katika miaka kumi ijayo kama kasi ya kupeana habari na kuwasiliana itaendelea kukua kwa kasi hii.Wewe binafsi unadhani tekinolojia imekusaidia vipi katika kufanikisha shughuli zako za kisiasa mpaka hivi sasa?

WS: Ni kweli teknolojia imesaidia sana. Hata hili unalofanya wewe ni msingi mkubwa sana katika kupeleka Taarifa kwa watu wengi zaidi. Hili lisingeliwezekana miaka takriban 10 iliyopita. Ninafurahi sana kwa maendeleo haya. Bunge la Tanzania lilipitisha, kupitia Miscellaneous Ammendement sheria kutambua Taarifa zinazopatikana katika Internet, lakini hatimaye Spika wa Bunge akapinga. Nadhani kuna haja kubwa viongozi wetu au kusoma na kupitia maamuzi ya nyuma. Viongozi wengi wanakosa Consistency kwa kusahau waliyoaumua wenyewe, au kupindisha tu sheria makusudi. Kama tunahitaji kwenda mbele ni lazima tuwe jamii yenye principles zisizoyumba na kubadilika badilika kama kinyonga.

BC: Sasa tungependa kukuuliza kuhusu chama cha CHADEMA.Wewe ukiwa kama katibu mkuu wa CHADEMA,unaweza kutueleza chama chenu kina visheni gani kwa taifa? Kama CCM imeshindwa, CHADEMA kinaweza kuwa chama mbadala? Kwa vipi?

WS: Misimao ya Chadema inajulikana wazi katika maswali mbalimbali. Ni dhahiri kuwa CCM imeshindwa kabisa kupiga vita Rushwa, Taifa kwa dhahiri limekosa mwelekeo katika mambo mengi, na CCM na Serikali yake hawataki kusikia, ili kujipongeza tu na miradi kama MMEM na MMES, ambayo kimsingi wala si sera yao ( imetokana na maamuzi ya Kimataifa ya kama vile MMEM na MMES ambayo yalifanyika Jomtien, Thailand, mwaka 1990). Hata hivyo, hatujatekeleza maamuzi hayo kama yalivyokubaliwa yaani EFA. Lakini CCM na Serikali zake kila siku wamekuwa wakijisifu bila kueleza chimbuko halisi la maamuzi hayo. Ndiyo maana hata upatikanaji wa fedha umekuwa rahisi kwa kiasi kikubwa. Mimi nimekuwa Makamu Mwenyekiti wa Afrika wa Wabunge wanaojishughulisha na Elimu, hivyo ninayafahamu kwa undani masuala haya.

 

Dr.Willibrod Slaa(katikati) akiteta jambo na Mwenyekiti wake,Freeman Mbowe(kushoto) na Zitto Kabwe,mbunge machachari wa Kigoma Kaskazini kupitia CHADEMA.

BC: Kumekuwepo na habari ambazo zimesambaa mtandaoni zikidai kwamba ndani ya CHADEMA pia kuna kashfa za ufisadi. Shutuma hizo zimekuwa zikielekezwa kwa Mwenyekiti wa CHADEMA na pia wewe mwenyewe.Unasemaje kuhusiana na shutuma hizi?

WS: Ni kweli kumekuwepo na taarifa kama hizo. Siwezi kumjibia Mhe. Mbowe, japo ninamfahamu Mwenyekiti wangu sasa kwa kiasi kikubwa. Na sijawahi kuona wala kushuhudia kinachosemwa. Hata hivyo:

Kwanza kusema au kutoa maoni ni haki ya watu wote. Tofauti ni kuwa hao wanaotoa maoni yao ni ya umbeya, au yanaushahidi kama sisi tunavyofanya? Mimi sina tatizo kama kuna tuhuma dhidi yangu ningelifurahi tu, zitolewe hadharani bila kificho na kwa ushahidi kamili.

Tuhuma zingine zinazoelekezwa Chadema kama za matumizi ya Helicopter, msingi wake tunaufahamu, na tusingelipenda kuwanufaisha watani zetu. Yatosha tu niseme hapa ni kweli, sisi tulikopa fedha kwa Mwenyekiti Mbowe kufanya kampeni zetu. Tuliweka taarifa zetu hadharani. Tukatoa changamoto kwa CCM watoe walipata wapi fedha zao hawajasema hadi leo. Swali la kujieleza, sisi tumekopa kwa Mwenyekiti wetu fedha za Helikopta, na tunamlipa kwa utaratibu uliokubalika kwa mujibu wa taratibu zetu.

Kwa ushahidi uliopo CCM kampeni wamefanya kwa fedha zetu, za Watanzania zilizochotwa BOT, Tangold, Meremeta kupitia DEEP GREEN, sasa nani bora? Nadhani mengine ni propaganda, na watu walidhani hatuna details ya tunayosema. Ninaendelea kui challenge CCM imepata wapi fedha za Kampeni na sources zao zilikuwa nini? Fedha zote zilizochotwa kupitia Deep Green Serikali na CCM lazima wazieleze zilienda wapi? Isitoshe, tulipoanza kutoa tuhuma, ni kwanini CCM walianza kuwakingia kifua watuhumiwa badala ya kuwaacha wajibu wao na au Serikali, lakini Katibu wa CCM anahusika vipi na tuhuma, kama dhamira yake haimsuti kuwa amegunduliwa na ndiyo taharuki ya kujibu hata yasiyomhusu na mwisho kuishia kwenye porojo na propaganda badala ya kujibu hoja?

BC: Ni kiongozi gani duniani anayekuvutia kutoka na jinsi anavyoongoza taifa au jamii yake?Kwanini?

WS: Kwa kuwa sijalifanyia utafiti naomba nisilijibu suali hili.

BC: Tukiachana kidogo na masuala ya siasa,unapokuwa mapumzikoni(tunaamini kwamba hufikia wakati ukahitaji mapumziko)huwa unapendelea kufanya nini?

WS: Nikiwa mapumzikoni mimi hupenda

1) Napenda sana kusoma vitabu mbalimbali vya Sheria, Siasa, maendeleo na hata Novels za kawaida.

2) Kujikumbusha lugha mbalimbali nilizojifunza nikiwa masomoni kama vile Kiitaliano, kijerumani, ili nisije nikazisahau.

3) Kutazama TV.

4) Kufanya shughuli za kawaida na kuzungumza na wapiga kura wangu jimboni.

BC: Mwisho una ujumbe gani kwa watanzania?

WS: Ningependa Watanzania watambue kuwa nchi ni yetu sote. Watanzania katika ujumla wetu ndio wenye nchi, Rasilimali zote za nchi ni zetu sote, na viongozi tumewapa tu dhamana ya kuzilinda kwa niaba yetu. Hivyo, tusiruhusu kabisa wakati sisi tunatumbukia kwenye lindi la umasikini wengine wananufaika kwenye migongo yetu. Kulinda mali zetu, ni jukumu la kila mmoja wetu pale alipo, kwa uwezo alionao na ufahamu wake. Ufisadi uko ngazi zote hadi vijijini tuukatae katakata popote pale. Rushwa tuikatae sote, na Mtanzania hata siku mmoja asikubali kununua haki yake iwe mahakamani, polisi, au hospitalini au popote pale ambapo huduma ni haki yake.

BC: Dr.Slaa,asante sana kwa muda wako.Tunakutakia kila la kheri katika shughuli zako.

WS: Shukrani sana,mimi pia nawatakieni kila la kheri.

 

50 Responses to ““TUUKATAE UFISADI”-DR.SLAA”

  1. Upendo Furaha Amani Says:

    Dr.Willibrod Peter Slaa, Ninakutakia kila la heri katika kazi yako ya kuwatetea Watanzania wanyonge. Ila jihadhari “wasije wakakumwagia tindikali” ili kukunyamazisha.
    Nawasilisha

  2. ntareyehirungu Says:

    Dr. Slaa, Mungu ndiye mlinzi wako na ndiye atakayekulipa kwa ujasiri wa kutimiza wajibu wako kwa Wadanganyika. Tupo pamoja nawe katika mapambano.

  3. Chris Says:

    He’s very objective. His response to the posed questions justifies that.

    Kama wengi wasemavyo, am also worried he may be assassinated, si unajua mafisadi walivyo. Lakini wasemavyo serikali impe ulinzi, serikali ya kifisadi, hakuna ulinzi hapo. Maana at the end lolote likitokea japo serikali inabidi iwe responsible/accountable but dont think if that will happen.

    Big up Brother, you are a true Tanzanian patriotic. We still need you alot,with our sprouting economy na rooting ufisadi.

  4. Majita Says:

    Uko hatua mbili mbele ya Uelewa wa CCM wote.
    Hongera na Mungu akuzidishie.
    Amen

  5. Nancy Says:

    Interview nzuri. kwa kweli maswali ni mazuri sana, lakini in my opinion, dr Slaa umeshindwa kuuza chama chako. Swali uliulizwa Chadema kinasvisheni gani kwa taifa? umeshindwa kabisa kutuambia what Chadema stand for, instead mnawa criticize CCM. Sasa tunajua kabisa CCM is corrupt, but what Chadema is going to do tukikichagua kama chama kiongozo cha TZ? Inabidi wana siasa wajue ku sell vyama vyao.

    Otherwise interview nzuri sasa BC tuletee mtu wa CCM nao wapate opportunity za kujitetea hoja alizozisema Dr Slaa.

  6. jossy Says:

    so many slaas are still required to sensitize Danganyikas who are far behind there rights.This painful of eunique tolerant Nation iam sure one day God will stand for it.GOD BLESS OUR NATION.GOD BLESS SLAA.

  7. UE Says:

    Tuko pamoja Dr, jitahidini kukijenga chama kwa kuwa na watu wenye uchungu na nchi hii, maana hao CCM watafanya kila njia ikiwa ni pamoja na kupanda watu ndani ya Chadema watakao wavuruga kama ilivyotokea kwa NCCR – Mageuzi na CUF.
    Mungu yupo atakulinda kamwe usirudi nyuma!!!

  8. Pope Says:

    Huyu ndiye “Raila” wa Tanzania, CCM mnamchekea ndio anakwenda hivoo, an reliable source of informations atawamaliza tuu. 2010 Si mbali shauri yenu.

  9. M-Mbea Says:

    Watu wamewashupalia BoT peke yao kwamba eti wamewaajiri watoto wa vigogo!
    Je Mmeona nyinyi hiyo listi ya WATOTO wa VIGOGO iliyoko kule TIC (Tanzania Investment Centre)?
    Hebu kaangalieni!

  10. john Says:

    me sina uhukika na ninyi wapinzani mnaanza kwa kasi afu mnatulizwa na ccm kwa kupewa chenu afu mnatambaa,yuko wapi zitto mbona hasikiki tena baada ya kuwekwa kwenye kamati ta madini,wanafki tu!mna interest zenu binafsi na ninyi mafisadi tu sema hamjapata nafasi!

  11. Matty Says:

    I like you hasa ulivyojieleza mh!!!!cv imetulia na kichwa kinafanya kazi sana!!!!!!lakini mungu ndiye anayekulinda katika maisha yako hasa unapotetea haki za wanyonge!

  12. mdunger Says:

    Mungu alipokutoa katika upadre kuja kwenye siasa ,ni kwamba ni wito mwingine,Ila jitahidini ninyi wa vyama mbadala(upinzani)mjiunge tuwape nguvu bungeni,msituangushe mkagawa kura,tuko wote1

  13. kahe stev Says:

    mzee wa watu kazi yako tumeiona na tunakuomba uendelee hivyo hivyo na sisi tunakuombea kwa aliye juu.Mungu azidi kukupa ujasili,nguvu pamoja na ulinzi wake.Amina

  14. mama Inno Says:

    Dr. Slaa nakufagilia keep it up utuokoe watanzania tusio na uelewa, Tunakuombea Uhai ili ufikishe jahazi hili pazuri zaidi, fichua uovu bila woga, Mungu yupo nawe milele yote.

  15. jozzee Says:

    nimependa interviw ya dr slaa hila kwenye cv yake ajaonesha kama amewahi kuwa padre lini maana nasikia alikuwa padre baadae akatafuna kondoo wa bwana pili mbona sijaona huo udoctor aliupataje? ajaeleza amesomea chuo gani otherwise he is good in this democratic coutry

  16. Liz Baraka Says:

    Dr. Slaa hongera sana. Bado nashangaa alipolipua bomu la mafisadi wa BoT, kuna watu wa ngazi za juu walianza kupinga, sasa mambo yako hadharani, wamekaa kimya, nahisi nao ni mafisadi wanapaswa kuangaliwa kwa macho mawili.
    Watanzania tumechoka kupelekeshwa, endelea kulipua uovu wowote utakaona ili mradi uwe na ushahidi.

  17. Dr. Slaa bravo. This is what patriotism is all about. Umeitanguliza nchi yako na watu wake mbele na si maslahi binafsi. Kwa mtaji huu wananchi sasa wanaanza kuelewa kuwa kama watachagua wapinzani wengi bungeni basi maslahi ya nchi na wananchi yatakuwa salama.

    Ninakuombea wewe na wenzako ili Mungu awalinde na mafisadi ambao weshajua kuwa sasa safari imewadia. Kwa uwoga wao uliopitiliza wako tayari hata kumwagia tindikali watanzania wenye uchungu na nchi yao. Mungu atawalinda usiku na mchana!

  18. Mbojeh Says:

    Kweli Dr. nakufagilia ipasavyo. Siyo tu kwa ajili ya maelezo yako ya kina ila kwa kuona kazi inavyofanyika kwenye jimbo lako la Karatu.

    You are the person ambaye unatakiwa kuishi ikiwezekana milele lakini najua haiwezekani. Ila wakati huu ambao Mungu bado anakutumia make sure that unasafisha huo ufisadi unaotumaliza watanzania. I believe that the Tanzania’s one day they will know all about, then they will stand for their right!!

    Msumari wa mwisho kwa hiki chama cha majambazi ni kwa uchaguzi wa jimbo la kiteto, tunaomba wote mhakikishe tunalichukua na kulimiliki.

  19. Burton Taibu Says:

    Kuna haja ya sisi wananchi kuunga mkono kwa dhati kazi za akina Dr Slaa na wengine. Njia moja wapo ni kuanza kujiunga kwa wingi kwenye vyama hivyo. Nina imani huu utakuwa mchango mkubwa wa kuanza kwa kuwaunga mkono, kama kweli tunayosema yanatoka mioyoni mwetu. Hii itawapa msukumo mkubwa wale wote waliojitoa mhanga kuwafagia mafisadi wa Chama Cha Mafisadi. Nakutakia maisha marefu Dr Slaa.

  20. Baraka Says:

    Slaa Mungu atakulinda tu, tuko nyuma yako. Tunawataka viongozi kama hawa Tanzania

  21. Mama wa Kichagga Says:

    Laiti kama kila Mbunge angekuwa chachu ya maendeleo katika Jimbo lake nadhani hata huu umaskini ungepungua kama si kuisha.

    Ni vyema viongozi/watendaji wakatekeleza sera za maendeleo jimboni/mahala pake pa kazi badala ya kuchukulia cheo kama sifa fulani tuu. Kuwa kiongozi hata ktk ngazi ya familia sio mchezo!

  22. CID Says:

    Dr. Slaa sio “whistleblower”!!!!

    Kasema yaliyokuwa yamejaa katika mtandao. kwa mfano, http://h1.ripway.com/Mwanakijiji/Maoni/tanzaniamafia.pdf

    Angekuwa “whistleblower” endapo angetwambia yanayofanyika ndani ya Chadema!

  23. M. Peter Says:

    NADHARIA THELATHINI KUHUSU UFISADI:
    UNAVYOJITENGENEZA, KUJILINDA, NA NAMNA YA KUPAMBANA NAO.

    Nadharia hii imeandikwa baada ya kutafakari matukio mbali mbali duniani yaliyotokea katika vipindi mbalimbali vya historia. Nadharia hii inajaribu kuchambua ufisadi pamoja na adhari zake na namna ya kupambana nao. Mwandishi alipoandika nadharia hii hakusoma kitabu au kazi ya mtu yeyote; wala hakuandika kwa mtiririko maalumu; bali alijaribu kutafakari na kuyaandika mawazo yake kama yalivyojitokeza ili kuchokoza mjadala, utafiti, au mchango zaidi kutoka kwa watu mbalimbali, ikiwa ni pamoja na wasomi, wataalamu wa sayansi ya jamii, na wahanga wa ufisadi. Lakini pamoja na kwamba nadharia hii ni ya awali, naamini inaweza kuwasaidia wana jamii kuufahamu kidogo ufisadi ulivyo na kufikiria namna ya kujipanga kupambana nao. Kwa watafiti na wasomi, itakuwa ni nafasi nzuri ya kuchambua zaidi, kutafiti na kuelimisha jamii zaidi juu ya adui huyu mkubwa wa mwanadamu.

    1. Ufisadi ni aina fulani ya tabia inayojitengeneza ndani ya moyo wa mtu mwenye asili ya uchoyo na ubinafsi.
    2. Ufisadi huanza kidogo kidogo katika maisha ya watu, hasa wale wanaopenda daima kuweka maslahi yao binafsi mbele zaidi kuliko ya wengine.
    3. Kama haupigwi vita mapema katika jamii, ufisadi unakua na kujieneneza; na kasi ya kukua kwake inaongezeka kama kuna watu wanaoshabikia ‘mafanikio’ yanayotokana na ufisadi huo.
    4. Ufisadi ulioachiliwa (ama kwa sababu ya hofu, kuoneana aibu, au vinginevyo) hujiimarisha kwa kujitengenezea mtandao wake mwenyewe.
    5. Mtandao wa ufisadi usipovunjwa mapema hukomaa na kutengeneza tabaka la mafisadi katika jamii, ambao hutafuta namna ya kuhalalisha ‘matunda’ ya ufisadi wao.
    6. Mojawapo ya njia inayotumika kuhalalisha matunda ya ufisadi ni kusaidia katika jamii, kutoa michango katika jamii au vyama, kuwekeza katika biashara, kusaidia wanasiasa kushinda uchaguzi, au kuingia serikalini; na ikibidi husaidia mafisadi wenzao kuingia kwenye siasa au shughuli nyingine muhimu.
    7. Wakati wote, tabaka la mafisadi huteteana kwa siri, lakini wakishajiona wamekomaa hukosa aibu hivyo huteteana kwa wazi. Na kwa hiyo fisadi mmoja hawezi kumwadhibu fisadi mwingine isipokuwa wamekosana katika mambo au maslahi yao
    8. Ufisadi uliojitengenezea tabaka huwa ni ngome ngumu kuivunja, kwani unatafuta mbinu zote kujilinda, kujitanua, na kujihalalisha.
    9. Ufisadi uliokomaa hauna huruma, aibu, wala staha. Na unakuwa mkali kwa wale wanaojaribu kuupiga vita.
    10. Mbinu kubwa ya ufisadi ni kusema uongo, kutumia vitisho, au kutumia nguvu yoyote ilioyokaribu nao (ya kipesa, kicheo, kichawi, kisilaha, kisiasa, kijeshi, kikabila, n.k.).
    11. Mbinu ya uongo ikishindwa, vitisho vinatumiwa, vitisho vikishindwa nguvu hutumika kutetea maslahi yao.
    12. Ufisadi ukipigiwa sana kelele na wananchi, unajipaka chokaa nyeupe kwa nje na kujifanya unaongoka, na hivyo kuwahadaa wananchi; kwa namna hiyo ufisadi hautenganishwi na unafiki.
    13. Unafiki wa mafisadi una mbinu tatu. Mbinu ya kwanza ni ya kujisafisha kwa juu juu pasipo toba la kweli. Hilo lisiposaidia, mbinu ya pili hutumika ambayo ni kuwachafua watu wengine waliosafi ili kuiaminisha jamii kuwa kila mmoja ni fisadi hivyo wasifuatwefuatwe. Hilo lisipofaa, mbinu ya nyingine hutumika ambayo ni ya kuwachafua baadhi ya mafisadi wenzao wachache, na hasa waliobainika, ili watolewe kafara na wengine wapate kupona. Mbinu zote zikishindikana, mafisadi wanaweza kudhuru watu ili kujitetea.
    14. Mtandao wa ufisadi unaweza ukawa wa sehemu moja kijiografia; au ukasambaa nchi nzima, na hata kuchukua sura ya kimataifa. Na unapovuka mipaka kuingia nchi nyingine, unatumia hila ya kuhadaa na kuwalainisha watu mashuhuri wa nchi au sehemu husika.
    15. Kama jamii ya wapenda HAKI na KWELI isipojizatiti na kupambana na ufisadi, na ukiachiwa utawale jamii kama unavyopenda, matokeo katika jamii yanakuwa ni mabaya sana. Jamii inakuwa mtumwa wa ufisadi, na mafisadi wanakuwa kama wafalme wa kudumu.
    16. Ufisadi unajidhihirisha katika sura mbalimbali kama vile rushwa kubwa na ndogo, ukandamizaji wa wanyonge, unyonyaji, kikundi kimoja kunyanyasa kingine, ubabe wa kiuchumi au kisiasa, biashara haramu (kama vile ya utumwa, madawa ya kulevya, bidhaa feki, biashara ya magendo, n.k.), uporaji wa mali na haki za wengine, demokrasia bandia, utawala mbovu, udikiteta, ajira mbaya kama vile ya watoto, n.k.
    17. Baadhi ya matokeo mabaya ya ufisadi ni kuongezeka unyonge na umasikini; kuporomoka maadili; chuki za kitabaka, kisiasa, kikabila, au kivikundi; vita vya wenyewe kwa wenyewe; mauaji ya kikabila, kikoo, au kisiasa; kukosa kuaminiana katika jamii, ukoloni wa sura mbali mbali, maisha ya wasiwasi, n.k.
    18. Kwa mantiki hiyo, ufisadi sio kitu cha kuchekea kabisa (hata kama unafanywa na ndugu wa kuzaliwa). Ni janga, aibu, na hatari kwa jamii au nchi yeyote ile. Pia ni ugonjwa mbaya unaoua kabisa maadili ya jamii, kwa maana vizazi vipya vinakosa mifano mizuri ya kuiga; pia vinakosa maongozi sahihi, licha ya kukosa haki zao za msingi na msaada wa kweli.
    19. Lakini jamii pia lazima ifahamu kuwa ufisadi uliokomaa hauwezi kujiondoa wenyewe, maana unajikita kama ufalme mdogo ndani ya jamii. Ili kupambana nao, umoja wa wananchi, nguvu, busara, na maarifa yanahitajika.
    20. Ufisadi hauwezi kupigwa vita na mafisadi, bali utapigwa vita na watu walio safi, wapenda maendeleo, haki, na kweli. Mwenye madoa ya kifisadi akipigana na mafisadi ataumbuliwa; ndio maana si rahisi kwa asiyesafi kupambana na mafisadi.
    21. Vita ya kupambana na ufisadi inatoka ndani ya moyo wa dhati wa mpenda haki, amani, na maendeleo ya watu; inahitaji uvumilivu, ni vita ya muda wote, haitafuti mafanikio binafsi.
    22. Vita ya kupambana na ufisadi inahitaji viongozi safi, wenye maono safi, wenye uadilifu, wanaoweze kuelezea umma malengo yao na kuhamasisha haki na kweli, na wanaoonyesha mfano wa kweli kupitia maisha yao wenyewe.
    23. Vita ya kupambana na ufisadi sio lele mama, ina hitaji kujitolea kwa hali ya juu. Lakini matunda yake ni mazuri, yanaleta faraja kwenye jamii, na yanadumu kwa muda mrefu.
    24. Kila mwana jamii aukemee ufisadi wakati wote na mahali popote anapouona, pasipo kujali kama ungemletea yeye faida fulani.
    25. Viongozi wa taasisi zote za jamii, serikali, kidini, na kitaaluma wapige vita ufisadi wa namna zote, na wahamasishe watu wao kuupiga vita ufisadi. Wanapofanya hivyo wajisafishe kwanza ili wawe mfano kwa wananchi wao wenyewe.
    26. Vyombo vya habari vina nafasi kubwa kusaidia wananchi katika vita hii, kwa kuendelea kufichua vitendo vya ufisadi, kuandika taarifa kwa busara, na kuhamasisha haki, kweli, na uadilifu katika jamii.
    27. Inawezekana kupambana na kuushinda ufisadi, unyonge, na umasikini kama wanajamii wakimaanisha na wakikusudia kujiletea maendeleo ya haki na kweli.
    28. Ikumbukwe kuwa ufisadi hauwezi kujiondoa wenyewe; wala malalamiko tu na kusimanga mafisadi haviwezi kuuondoa ufisadi. Wala ushabiki tu wa juu juu hauwezi kuuondoa ufisadi. Kinachohitajika ni juhudi na nguvu za dhati na za pamoja kati ya wananchi na viongozi wao, pamoja na taasisi za dini na zile zinazotetea haki za watu.
    29. Kwa kuwa ufisadi unatumia mwanya wowote na hasa udhaifu fulani katika jamii, ni vema kuhakikisha kuwa maeneo yote ya kijamii yanaboreshwa (kama vile sheria za nchi na serikali za mitaa, kanuni na taratibu za taasisi, utendaji wa vyombo vya kusimamia haki na sheria, utawala bora, utendaji wa vyombo vya habari, demokrasia na ushirikishwaji umma, maadili ya viongozi, n.k.)
    30. Ili kusaidia vizazi vijavyo, elimu na itolewe kuanzia ngazi ya shule za msingi. Elimu hiyo ilenge kuwasaidia vijana kuwa waadilifu, kuuchukia na kupambana na ufisadi. Kama vile tunavyopambana kulinda mazingira yetu, ni lazima kupambana pia kulinda jamii zetu na utu wetu. Mazingira ni muhimu, lakini ni kweli pia kuwa utu wetu ni muhimu zaidi. Maana utu wetu ukiharibiwa, na jamii ikiharibiwa na ufisadi, je mazingira hayo yatamsaidia nani?

  24. george Says:

    dr.slaa hakika wewe ni kiongozi wa kweli abaye taifa linakutegemea kwa ajili ya kuleta maendeleo.pia wewe ni kiongozi wa kweli na mkombozi wa wanyonge

  25. […] “TUUKATAE UFISADI”-DR.SLAA [image]Jina la Dr.Willibrod Peter Slaa (pichani),Katibu Mkuu wa CHADEMA na Mbunge wa Karatu, hivi sasa linaweza kuwa […] […]

  26. mstari mbele Says:

    MUNGU akutangulie dr.Slaa na km waliotangulia kwa kusema ya kua kakutoa kwenye upadri,basi naamini siasa ni wito mwingine,na km ulivyosema ya kua Mungu pekee ndio mlinzi wako ni kweli kabisa,ivyo basi nawaomba vijana wenzangu wa kitanzania popote pale tulipo tuweze kuyaona na kuyasikia haya ili hata sisi ikifikia wakati wa kuchukua nchi tubadilishe nchi yetu yenye kila aina ya utajiri,ila wananchi wake bado maskini,najua watoto wa mafisadi hamuwezi kunielewa sababu wazee wenu ndio wanapopata hela za kuwapeleka masomoni ulaya,na marekani,ni bora basi mkapewa skolashipu za watu wengine then mkasoma,ila mkifika huku ni upuuuzi mtupu mnafanya,ni bora wangepewa wale walengwa wangesoma na kwenda bongo kubadilisha nchi yetu,Mungu mbariki Dr.Slaa na ibariki tanzania.

  27. Mr Tom Says:

    Mimi shida yangu ni kwenye elimu. Huyu Mh. anaitwa Dr.Sasa ninavyojua mimi kuitwa Dr.ni lazima uwe na sifa zifuatazo
    1.Shahada ya Udaktari wa Falsafa(PHD)
    2.Uwe na shahada ya kwanza aidha ya udaktari wa binadamu(MD) au wa mifugo(VD)
    3.Na mwisho ni udaktari wa heshima unaotokana na Chuo Kikuu chochote duniani kutambua mchango wako kwa jamii kama ilivyowahi kutokea kwa Rais mstaafu Benjamini Mkapa,mzee Marecela,katibu mkuu wa zamani wa UN bwana Kofi Annanna hata Rais Kikwete hivi karibuni alipewa heshima hiyo ya udaktari wa falsafa hivi karibuni na chuo kikuu kimoja hapa Marekani.Na wengine wengi tu. Sasa nikiangalia wasifu wa Mh.Slaa kuhusu kipengere cha elimu sioni hata moja ya sifa hizo zaidi ya kuona mlundikano wa Diploma na cheti tu.Naomba ndugu uliyehusika kufanya mahojiano haya unisaidie katika hilo na sijui kwanini ulisahau kuuliza swali hilo muhimu sana.Mara kadhaa nimekuwa najiuliza udaktari wake maana najua alikuwa padiri.

  28. Mselema Says:

    Dr, you are a MAN, GOD Bless you.

  29. samwel john Says:

    Mh.Dr.Wilbroad Slaa.Ninakupongeza kwa hatua yako ya kutuamsha sisi tulio ktk usingizi mzito,ni kiwa nina maana kuwa haya tusingeyajua bila ya wewe kutueleza kwa kina,hii n kuonyesha kuwa unazalendo na nchi yetu.Nionavyo mimi vita dhidi ya ufisadi bado ni kubwa na inayojitokeza kila kikichwa mfano Mibuzwagi,TICTS.Tukiungana kwa pamoja vita dhidi ya ufisadi itatokomea.Aluta Continua

  30. nyesi Says:

    All what I can say is go, go, go Dr Slaa, be a good siraha to all Tanzanian, as your name sound!

    We love you and pray for you.

  31. chikala Says:

    Dr.Usikate tamaa wanao kubeza ni ndugu na mafisadi hao kwa namna moja au nyingine wananufaika kiujumla.

  32. Chakoma Says:

    Kandamiza mwanawanye

  33. Bongo Pixs Says:

    Zidi kufichua bado uozo ni mwingi sana hii ni sehemu tu.

  34. Stranger Says:

    Your defenition of whistleblower is wrong, if he was government employee and work on the government department where there is wrong doing and go public against a department wishes then yes.

  35. Terri Moses Says:

    Stranger,
    Kuna tofauti kati ya whistleblower na whistle blower.Whistleblower kama ilivyotumiwa na BC maana yake ni –noun
    a person who informs on another or makes public disclosure of corruption or wrongdoing.

    Huelewi au unajifanya tu mjuaji ili nawe uonekane unajua?By any standards and definitions Dr.Slaa is a whistleblower.Hakuna makosa ya kimsingi kumuita Dr.Slaa whistleblower.Watu wengine bwana kujifanya wajuaaaajiiii,mnakera.

  36. Kiboko ya wamama Says:

    1979-1981 Pontifical Urba University,Rome,JCD(summa cum laude)
    His PhD

  37. ochumale Says:

    huu uchunguzi wenyewe ulikuwa kwa shinikizo la wahisani na wala si serikali yetu ya Kikwete. mkaguzi mkuu alikuwa anafanya nini siku zote? mbona alikuwa haoni huo wizi lakini Dr. Slaa kauona tena bila hata kukagua hayo mahesabu kama yeye. shame on you government of tz

  38. tonny Says:

    Tungekuwa na Dr.Slaa watatu tu hapa nchini,viongozi wetu wangekuwa wanausikia Ulaji kupitia CNN tu!Viongozi wangenyooka na kutambua kwamba kuwa kiongozi siyo tiketi ya Ulaji mwanangu!Kiongozi utatakiwa uongoze njia katika mema!Wewe ni Mkombozi wa Wanyonge.Mungu daima atakulinda kwa hilo.Mhalifu hata awe na pesa kiasi gani ni kiumbe mwoga sana kama mlikuwa hamjui.Dawa yake akijulikana tu,basi biashara imekwisha wazee!

  39. Gody Says:

    Dr. Slaa, nakupongeza/nawapongeza sana kwa juhudi mnazoendelea nazo za kuhakikisha inchi nzima anakuwa na uelewa wa kile kinachoandelea ndani ya serikari ambapo itapelekea watu kuchagua viongozi wenye kupigania mslahi ya taifa na raia kwanza.

    Inauma sana kwani watanzania wana hali mbaya ambayo huwezi kulinganisha na ya viongozi wao na hakuna mikakati au uashilia wa kwamba siku moja mambo yatakuwa safi zaidi ya kuwa magumu siku hadi siku, kitu ambacho naona hawa watu hawana huruma kabisa EEh jamani..!!!!!!!!!!!!.Naomba msikate tamaa msikubali hongo maana ndo mchezo wao, msikubali watu kuingia ingia kwenye chama huenda wakawa ndo wale wapandikizwaji wa kuvuruga na mwisho nasema tuko pamoja na Mungu ndio Mlinzi wetu Kila la heri.!

  40. Nyosa Says:

    Ukweli Mh Dr Slaa umeonyesha uzalendo wa kweli.Usiogope maneno ya watu.kumbuka wawekezaji kwenye biashara ya utumwa enzi hizo.Walisaidiwa na watawala wetu na pia kulikuwa na watu ambao waliupinga na ndugu zao waliokuwa wakinufaika walishindwa kuwaelewa na ikiwezekana walishirikiana na wawekezaji wa utumwa kuwaua waliopinga.Hali haijabadilika sana ila bidhaa ndiyo iliyo badilika.Ukisema mungu atalipa bado dalili hizo hazipo,Ila ni kwa watu kama wewe kuchukua hatua uliyo chukua kwani umeonyesha njia na uongozi ni ujasiri na kuonyesha njia.Endeleza mapambano

  41. Dr Mtei Bonaventure Says:

    Mh. Dr Slaa,
    Naungana na Watanzania wengi wanaokusifu kwa ushujaa wako. Aksante sana kwa kujitolea mhanga kukemea ufisadi nchini Tanzania. Naamini ujasiri wako utapelekea Watanzania kuondokana na tabia iliyojengeka miongoni mwa jamii ya kukumbatia ubadhirifu, wizi na maovu ya kila aina. Huo ndio ukombozi kwa Mtanzania wa leo anayegubikwa ndani ya umaskini uliokithiri.

  42. Huu Ndio uzalendo halisi ambao watanzania wote tunatakiwa kuwa nao,kama alivyofanya Dr Silla, kakataa rushwa kuanzia kwenye moyo wake hadi matendo yake.

    Nakufagilia Dr Silla, Zitto Kabwe na The Chadema Cabinet.

  43. CID Says:

    Mr Tom Says: January, 29, 2008 at 12:56 am, umeandika pamoja na “Shahada ya Udaktari wa Falsafa

    Shahada za udaktari (doctoral degrees) ni nyingi. Mojawapo ni hiyo ya PhD. kwa mfano tu, mtu anweza kuwa na PhD in Education. Mwingine akawa na D.ED. Kuna PhD ya Sheria na JD.

    Hebu waulizwe walimu wafundishao doctoral studies wakuelemishe.

  44. 15. Jozzee
    Ndugu yangu huwezi kuwa Vicar General kama si padre……huyo ni msaidizi wa Askofu kama hujui tena Kanisa katoliki
    Na kama umefuatilia kwa makini CV yake utaelewa tu Mh. alikuwa kwenye mkondo wa kanisa
    Nafikiri umenipata Jozzee……
    Tukubali tu Dr Mtanzania Halisi katutoa LIVE
    wacha mafisadi wazidi kupata mastress na sasa watalazwa TEMEKE HAKUNA CHA LONDON WALA UK

  45. amsi Says:

    Dr Slaa ni mwanamapinduzi,anayesimamia katika kweli na haki.Anafaa kuigwa na Watanzania,hususan vijana.

  46. frank abel Says:

    Dr slaa anasitahili pongezi zote kwani walikuwepo wengi walioyajua hayo hata kama yalikuwa kwenye mtandao rakini hawakuyasema.big up slaa

  47. BEN Says:

    MZEE sijui nimwombe mungu akupe baraka gani maana unachokifanya si kwa ajili ya kizazi hiki tu bali ni kwa watanzania wote hata hao wanaojiita makada wa CCM maana nchi ikenda mlama hata wao watathilika sana kwani watakosa hata cha kuchukukua
    MUNGU IBARIKI TANZANIA ,MUNGU MBARIKI DR.SLAA
    AMEN

  48. BEN Says:

    kama nchi hii itapata watu kumi wenye uchungu kama wa huyu DR. nchi inaweza kufikia mahali pazuri maana bila ya wafia nchi hakuna atakaye weza kuikomboa nchi labda tumlilie Mungu aturejeshee baba wa Taifa letu .Dr.na wenzako tusaidie fumbueni macho ya watanzania maana giza bado limetanda .Tusingoje uchaguzi maana muda hautatosha kuelimisha umma .wenzetu wanasonga kwa stali ya kuwasema mafisadi jukwaani huku wanakula nao kwenye vikao vyao vya kula kuku na kupongezana kwa kutuibia

  49. liza Says:

    Dr. Slaa Mungu akuzidishie siku za kuishi maana unatusaidia sisi wanyonge wa mlo mmoja kwa siku, angalau kwa kusema yote hayo tunapata ahueni ya kujua kwamba unatuonea huruma, achana na hao wanaotaka kujua kama wewe ni dr, au la tena hao ni wa CCM achana na hao mafisadi, wanaokuponda usiyasikilize wewe kaza buti mzee.
    Nakutakia kila la heri mzee endeleza libeneke usitishwe na yeyote kwani Mungu ndiye kinga yako!


Leave a reply to BEN Cancel reply