Hatimaye siku 365 za mwaka 2008 zimefikia ukingoni.Ninavyoandika ujumbe huu tayari kuna sehemu mbalimbali za dunia ambapo tayari sekunde za mwisho za mwaka huu zimeshahesabiwa na tayari takwimu mpya zimeshaandikwa.Kwa maana hiyo leo ni mwaka mpya. Kwa heri mwaka 2008 karibu mwaka 2009.Kwa wengi leo huwa ni siku nzuri kwa maazimio mapya ndani ya matumaini mapya.Kwa jinsi hali ya uchumi duniani ilivyoishia mwaka tunaoupa kisogo,basi sio ajabu kwamba malengo ya wengi ni kulinda zaidi mifuko yetu kwa kuwa makini zaidi na matumizi hesabu za mapato na matumizi na pia kulinda zaidi kazi zinazotuingizia kipato.Nakutakia kila la kheri katika hilo.
Bila kujali hali ya kiafya,kiuchumi,kisiasa wala kijamii, ukweli kwamba mwaka mpya umewadia huku wewe na sisi sote hapa BC tukiwa hai, ni jambo la kufurahia na kumshukuru Muumba.Ukivuka mwaka unakuwa umeandika historia mpya katika maisha yako. Vitabu vya kumbukumbu vitaandika kwamba uliuona mwaka 2009! Ni jambo la kumshukuru muumba kwani ni wazi wapo wengi sana waliotamani kuuona mwaka huu na wasifanikiwe.Kama huamini, fikiria kidogo tu ni watu wangapi ambao umehudhuria mazishi yao au kusikia habari juu ya misiba yao?Unaona? Hatuna budi kumshukuru Mungu.
Wakati huu tunapoingia mwaka mpya wa 2009,tungependa kwanza kukutakia kila la kheri wewe msomaji,mtembeleaji au mchangiaji wetu.Mwenyezi Mungu akuongoze na kukubariki katika kila jambo utakalolifanya ndani ya mwaka huu wa 2009.Kama mwaka 2008 haukuwa wenye mafanikio kwako au haukutimiza malengo yako,usikate tama.Fungua ukurasa mpya huku ukiwa na fikra chanya zaidi na utaona mabadiliko.
Tungependa pia kukupa shukrani zetu za pekee kwa kuwa mtembeleaji,msomaji au mchangiaji mzuri wa BC.Kama kuna mafanikio yoyote ambayo tumeyapata tangu kuanzishwa kwa blog/site hii,ni wazi kabisa kwamba mafanikio hayo yametokana na mchango wako wewe msomaji,mtembeleaji na mchangiaji wetu.
Shukrani nyingi ziwaendee celebrities mbalimbali ambao bila maringo,kinyongo wala ngendembwe walikubali aidha kufanya nasi mahojiano au kutokuwa na kinyongo nasi pale tulipoweka picha zao na kukaribisha mvua ya maoni kutoka kwa wasomaji huku wengine wakiwa chanya na wengine hasi.Celebrities kama hao wanakuwa wametambua vyema nafasi au mchango wao katika jamii.Wametambua pia kwamba haiwezekani kuwa bondia ulingoni halafu ukawa unaogopa ngumi za uso.Tunawashukuru na kuwaomba tuendelee kushirikiana.
Shukrani za pekee ziwafikie bloggers wenzetu mbalimbali,vyombo mbalimbali vya habari ndani na nje ya Tanzania,wapiga picha mbalimbali na wengineo wote ambao wanaendelea kushirikiana nasi katika jukumu hili zito la habari na mawasiliano.Asanteni sana.Bila ninyi,haiwezekani.BC inathamini sana mchango wenu.
Kama binadamu inawezekana kabisa kuna wakati tunatokea kutoelewana au hata kukwazana.Bila shaka hata sisi hapa BC inawezekana kuna wakati tulikukwaza.Yawezekana hatukuweka maoni yako kwa sababu moja au nyingine,yawezekana tulichelewa kuruhusu maoni yako yaonekane,yawezekana wewe ni celebrity na tuliruhusu maoni ambayo kimsingi uliona kama umetusiwa nk.Mifano ipo mingi.Lakini kwa wote hao,tunaomba samahani.Yote hayo ni katika kujitahidi kuitenda vyema kazi yetu.
Tunapouanza mwaka mpya wa 2009,tunakusihi uendele kututembelea,kuchangia,kutukosoa tunapokosea na pia kumwambia mwenzako kuhusu uwanja huu ili naye asipitwe na yanayojiri.Tunakutakia kila la kheri.HAPPY NEW YEAR 2009.
Recent Comments